MIFUKO HIFADHI YA JAMII ISIGEUZWE UPATU – WATAALAMU

 

*Wasema “itakuwa kama DECI – wastaafu wa sasa kutakata, wa kesho chali” 

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

UNAWEZA kushangaa pale ambapo Shirika la Kazi Duniani, ILO, linawalalamikia viongozi wa Chama cha Wafanyakazi Tanzania, TUCTA, kwamba wanaua mifuko ya hifadhi ya jamii nchini, baada ya kupandisha kikokotoo.

Kwa nini ILO wawalalamikie TUCTA wakatii kikokotoo kimepanda juu sana kuliko taifa lolote duniani, hata kuyazidi mataifa yote yenye uchumi mkubwa zaidi duniani kama Marekani, China, Ujerumani, Uingereza, Japan, Ufaransa na hata Afrika ya Kusini?

Shirika la kazi Duniani liliona Kikokotoo cha asilimia 50 kilikuwa kinakwenda kuifilisi mifuko ya hifadhi ya jamii. ILO wenyewe wakalalamika. Hata Kikokotoo chetu cha sasa cha asilimia 33, ILO wametuweka kwenye uangalizi (red flag).

Hata hivyo, kwa huruma tu, tunaweza kupanda kidogo, iwapo Serikali itaamua kuingiza fedha zake, jambo ambalo linahitaji uangalifu mkubwa. Labda elimu ya kina itolewe kwa watanzania na wapotoshaji wadhibitiwe.

Ongezeko dogo linaweza kuwa himilivu kwa ufadhili wa Serikali, kiubishi, kwa ubinadamu tu, lakini pia kwa uangalifu mkubwa sana.

“Wakati mifuko inaunganishwa, uhai wa mfuko wa PSPF uliokuwa unalipa kikokotoo cha asilimia 50, ulikuwa umebakia miaka 11 tu ufe. Hii ina maana kuwa, baada ya miaka 11, kusingekuwa na mfuko wa pensheni wa watumishi wa umma. Ukwasi wake ulikuwa taabani,” alisema mbobezi wa hifadhi ya jamii nchini, Dkt. Aggrey Mlimuka.

Wakati PPF na NSSF zilizokuwa zinalipa kwa kutumia Kikokotoo cha asilimia 25, zilikuwa na uhai wa maelfu ya miaka. Hivyo, kuijumuisha mifuko na kurekebisha kikokotoo, kumeuongezea mfuko huu uhai wa miaka mingi zaidi.

Wabobezi hao walikuwa wakiongea katika mjadala wa Kikokotoo uliofanyika kwa kutumia mtandao wa kijamii.

Wakumbushia Majuto ya Malipo Makubwa ya Mkupuo

“Sisi wengine tulionja chungu ya “provident fund,” mifuko ya akiba (ni tofauti na mifuko ya pensheni, kwenye akiba unatunza na kupewa ulichoweka na kifaida kidogo) na mkupuo wa mara moja. Ni wale tuliorithi mfuko wa University of East Africa ulioitwa Senior Staff suprennuation Scheme (SSSS),” alionya Mwanazuoni mmoja mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Aliendelea, “usiombe! Afadhali sisi waajiriwa wa 1976 na 1977, tuliokolewa kwa kuongezewa ruzuku ndogo na Serikali kupitia PPF. Waliotutangulia walilia sana. Mkupuo mmoja ni mbaya sana,” aliongeza.

Mhadhili huyo mstaafu aliyeandika vitabu vingi vya kitaaluma na mshauri wa kimataifa, alisema kujadili ongezeko la mkupuo si vibaya, lakini mantiki inaelekeza ongezeko hilo lisiwe kubwa ili malipo ya kila mwezi baadaye yawe na maana,” aliongeza.

Wahenga walisema uzee dawa. Dkt. Mlimuka, sasa mstaafu, lakini anayetumika kushauri mifuko ya hifadhi ya jamii,  mwenye miaka mingi ya uzoefu katika sekta ya hifadhi ya jamii, nchini na nje ya nchi, alikumbushia yaliyotokea miaka ya nyuma.

“Baadhi ya wafanyakazi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), waliokataa kujiunga na PPF ili wapate pensheni ya kila mwezi, mpaka leo walikuwa wanajutia maamuzi yao,” alisema.

Aliongeza kwamba, wafanyakazi hao, wengi wakiwa wahadhiri, walichagua kuendelea na mfuko wa akiba wa SSSS, ambapo walipata mkupuo mmoja mkubwa na hawana pensheni hadi leo.

“Kwa mfanyakazi aliyezoea kupata mshahara wa kila mwezi, pensheni nzuri ya kila mwezi ni bora kuliko malipo ya mkupuo, ambayo mara nyingi huisha mapema,” aliongea kutokana na uzoefu wa tasnia hiyo.

Naye mtaalamu wa sayansi ya mahesabu (Actuarial Scientist), Phostine Oyuke, alitoa ushauri kwa waastaafu watarajiwa.

“Wenzangu ambao tuna miaka 10-20 kustaafu, tukijaaliwa, tunadhani mkupuo ni suluhu. Provident funds hazijawahi kusaidia kwenye stability ya social security popote. Haya mambo yamefanyiwa tafiti duniani kote,” alisema.

Bw Oyuke ambaye ni Actuarial na amebobea katika fani ya bima, aliongeza, “Niseme tu, iwapo mtu anataka kikokotoo kipande zaidi ya hapo, maana yake, anataka kuigeuza mifuko ya hifadhi ya jamii kuwa upatu, “ponzi schemes”, yaani wachangiaji wa mwanzo wapate wa mwisho wakose,” aliongeza.

Bw Oyuke alisema wastaafu wataathirika sana iwapo, baada ya kutafuna mkupuo wote, wakiwa hawana kipato cha kukidhi walau mahitaji yao ya kila siku.

Hifadhi ya Jamii sio UPATU

Mtaalamu huyo alisema kuwa hifadhi ya jamii haipaswi kuwa UPATU (pyramid Scheme) kama ilivyokuwa DECI. “Watu wazima tunakumbuka wazazi wetu walilipwa mkupuo mmoja, lakini walilalamika ili walipwe kidogo kidogo,” alikumbusha.

Mwanasayansi huyo alitabiri kuwa, iwapo kikokotoo kitapanda na kulipa kiinua mgongo cha asilimia 50, upo uwezekano kuwa ndani ya miaka 7 hadi 10 hakutakuwa na mifuko ya hifadhi ya jamii.

“Mimi sina tatizo na kikokotoo cha asilimia 33, ni kizuri na wapo wafanyakazi wengi wake comfortable [wanaridhika] nacho, ikifika tarehe 25 ya kila mwezi, muamala unasoma,” alisema Bw Junus Ndaro, Katibu Mtendaji wa Chama cha Wafanyakazi wa Sekta ya Mtandao wa Mawasiliano Tanzania (TEWUTA).

Wastaafu walikuwa wanasubiri hadi miaka mitatu bila kulipwa

Mwanasayansi mmoja mwenye uzoefu wa hifadhi ya jamii nchini alibainisha kuwa, kabla ya kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii mwaka 2018, mfuko wa PSSSF ulikuta wanachama elfu kumi (10,000) waliokuwa wanalipwa kwa kikokotoo cha mkupuo cha asilimia 50, wanasubiri kulipwa kwa zaidi ya miaka miwili hadi mitatu baada ya kustaafu.

Mtaalamu huyo ambaye pia ni actuarial, anasema kuwa baada ya kushusha kikokotoo hadi asilimia 33, sasa wastaafu wanasubiri mafao yao kwa siku 60 tu na juhudi zinaendelea kufanywa ili walipwe mkupuo wao ndani ya siku 30 tu baada ya kustaafu.

Hii ni kwa sababu kikokotoo cha 33 ni himilivu. Kikokotoo kikiwa kikubwa sana kuliko uwezo, wastaafu wanaweza kurejea kwenye hali ya zamani ya kusubiria kwa miaka, wakisugua lami, kama ilivyokuwa akina mama wakisubiria maji ya chemchem kisimani yajae ili wachote.

“Watanzania wanapotoshwa na baadhi ya wanasiasa wasio wataalamu wa mahesabu,” alisema mmoja wa walimu walioshiriki semina ya kikokotoo, Mwalimu Joseph Laurenti wa Arusha.

Mikupuo Ilivyowatesa Wastaafu wa Kiltex

Miaka kadhaa iliyopita, walikuwepo wastaafu wa kiwanda cha nguo cha Kilimanjaro (Kiltex) ambao kwa wakati huo, waliruhusiwa kuchukua fedha zao zote.

“Bila hiana, nao walichukua, wakaondoka kwa furaha tele na bashasha za kutosha. Baada ya mwaka mmoja, wote wakarudi kwa umoja wao, wakiomba warudishwe kwenye pensheni ya kila mwezi, wakaambiwa kuwa hilo lisingewezekana kwa kuwa walishachukua fedha zao zote, wakalalamika sana maisha magumu. Hadi leo bado wanalilia jambo hilo,” alisema Dkt. Mlimuka ambaye kwa miaka mingi alikuwa Mtendaji Mkuu wa chama cha waajiri Tanzania (ATE).

“Mimi ninayepokea pensheni ya kila mwezi, hata ukiniambia leo nipewe fedha zilizobaki, siwezi kukubali, kwa kuwa ninajua adha ya mkupuo na raha ya kupokea pensheni kila mwezi,” aliongeza mbobezi huyo.

Mwandishi wa Makala haya ni mchangiaji wetu na mtafiti katika eneo la hifadhi ya jamii. Anapatikana jijini Arusha, Tanzania.

Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"