Na.
Saidina Msangi na Peter Haule, WF, Dodoma
Katibu
Mkuu Wizara ya Fedha Dkt. Natu El- Maamry Mwamba, amesema Shirika la
Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA), kupitia mpango uliotiwa saini mwaka
2014 limetoa ruzuku ya jumla ya Dola za Kimarekani milioni 139.5 sawa na Sh.
bilioni 356.3 kwa Tanzania kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya
maendeleo.
Dkt.
Mwamba alibainisha hayo jijini Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na
Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea anayeshughulikia
mambo ya kimkakati (KOICA) Don Ho Kim, aliye katika ziara ya kikazi Tanzania.
Alisema
kuwa kupitia fedha hizo miradi kadhaa imekamilika na mingine inaendelea ambayo
ni pamoja na Mfuko wa sekta ya Afya na
Mpango Jumuishi wa Vijana Walio nje ya Shule (IPOSA).
‘‘Miradi
kadhaa iko katika hatua mbalimbali za maandalizi, ikiwa ni pamoja na kuanzisha
mifumo ya usambazaji maji kwa maeneo ya mijini na vijijini mjini Dodoma na
kuboresha usawa wa kijinsia katika Elimu (STEM) kwa Shule za Sekondari nchini
ambapo miradi hii kwa sasa inapitia michakato ya kuidhinishwa ndani ya Wizara
husika’’ alisema Dkt. Mwamba.
Alisema
tangu 1991, KOICA imesaidia Serikali hasa katika nyanja za afya, elimu, maji na
usafiri ili kubadilisha hali ya kijamii na kiuchumi nchini.
Dkt.
Mwamba alisema kuwa kupitia mipango mbalimbali ya ufadhili, usaidizi wa
kiufundi na programu za kujenga uwezo, KOICA imechochea mabadiliko chanya na
yaliyosaidia ukuaji na ustawi jumuishi, kupambana na umaskini na kukuza uchumi.
Aidha
alieleza kuwa Agosti 2023, Wizara ya Fedha iliwasilisha ombi la miradi minne ya
maendeleo kwa msaada wa KOICA ya jumla ya Dola za Kimarekani milioni 39, sawa
na Sh. bilioni 98, inayotarajiwa kutekelezwa
kuanzia mwaka 2025.
Dkt.
Mwamba alibainisha miradi hiyo kuwa ni mradi wa kuanzisha chuo cha ufundi Morogoro, mradi wa kuimarisha huduma za mama na mtoto
jijini Dar es Salaam, mradi wa kuanzisha mifumo ya usambazaji maji katika
maeneo ya vijijini vya mkoa wa pwani na mradi wa kuanzisha mpango kabambe wa
kitaifa wa barabara kuu na uboreshaji wa uwezo wa rasilimali watu.
Dtk.
Mwamba aliishukuru Serikali ya Jamhuri
ya Korea kupitia KOICA kwa kuunga mkono malengo hayo ambapo imekuwa mojawapo ya
vyanzo vikuu vya ufadhili wa ruzuku katika kufanikisha miradi ya maendeleo na
kusisitiza kuwa Tanzania itaendelea
kuhakikisha kuwa rasilimali zote zinazopatikana kutoka KOICA zinatumika
kwa uangalifu ili kufikia malengo yaliyokusudiwa ndani ya muda uliokubaliwa.
Kwa
upande wake Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea
(KOICA) Don Ho Kim, alisema kuwa Korea itaendelea kushirikiana na Tanzania
katika maendeleo ya uchumi hasa katika ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji,
afya pamoja na kuwezesha wafanyabiashara wadogo kuweza kunufaika na masoko.
Kuhusu
miradi iliyowasilishwa na Tanzania alisema kuwa, ipo katika mchakato wa
kuidhinishwa na Shirika hilo ambapo kati ya Novemba na Desemba mwaka huu
inatazamiwa kuidhinishwa na Bunge la nchi hiyo, aliahidi nchi yake kuendeleza
ushirikiano na kuunga mkono mipango ya maendeleo ya Tanzania
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akimkabidhi zawadi yenye picha ya Mlima Kilimanjaro, Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA) anayeshughulikia mambo ya kimkakati, Mhe. Dong Ho Kim, baada ya kumaliza kikao kilichojadili ushirikiano na utekelezaji wa miradi ikiwemo ya miundombinu, elimu na afya, kilichofanyika jijini Dodoma.
Ujumbe kutoka Tanzania ulioongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba (kushoto) na ujumbe kutoka Jamhuri ya Korea uliyoongozwa na Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA) anayeshughulikia mambo ya kimkakati, Mhe. Dong Ho Kim ukiwa katika mkutano ulioangazia ushirikiano wa maendeleo, kilichofanyika jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry
Mwamba akizungumza kuhusu miradi ya maendeleo wakati wa kikao na Makamu wa Rais
wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA) anayeshughulikia Mambo
ya Kimkakati Mhe. Dong Ho Kim, jijini Dodoma.
Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa
Kimataifa la Korea (KOICA), anayeshughulikia mambo ya kimkakati, Mhe. Dong Ho
Kim, akizungumza wakati wa kikao na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu
El-Maamry Mwamba ambapo alisema kuwa Korea itaendelea kushirikiana na Tanzania
katika utekelezaji wa miradi mbalimbali, kilichofanyika jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry
Mwamba, akiagana na Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la
Korea (KOICA) anayeshughulikia mambo ya kimkakati, Mhe. Dong Ho Kim, baada ya
kumaliza kikao kilichojadili ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Korea
katika utekelezaji wa miradi mbalimbali, kilichofanyika jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry
Mwamba (watano kulia), na Makamu wa Rais wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa
la Korea (KOICA), anayeshughulikia mambo ya kimkakati, Mhe. Dong Ho Kim (wasita
kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe kutoka Wizara ya
Fedha na ujumbe kutoka Korea (KOICA), baada ya kikao kilichojadili kuimarisha
ushirikiano, kilichofanyika jijini Dodoma.