8/31/2021
WAZIRI MKUU AZINDUA TAWI LA BENKI YA MWANGA NA KUTOA MAAGIZO SABA
MAJALIWA: SERIKALI KUBORESHA MIUNDOMBINU YA VYOMBO VYA ULINZI NA USALAMA.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo Agosti 30, 2021 amefungua majengo ya Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Singida na Ofisi za Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia Mkoa wa Singida, miradi ambayo imegharimu shilingi bilion 1.314
Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Waziri Mkuu amesema kuwa amefurahishwa na mradi huo ambao ujenzi wake umetumia muda mfupi na umeokoa kiasi kikubwa cha fedha za Serikali. Ameahidi kuwa serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya vyombo vya ulinzi na usalama.
“Nawapongeza sana wasimamizi wa mradi huu kwa kuhakikisha unatekelezwa vema na kuakisi thamani ya fedha za mradi yaani value for money sanjari na kukamilika kwa wakati. Tumeelezwa hapa kuwa mradi huu uliotekelezwa kwa mfumo wa nguvu kazi yaani force account, ulianza tarehe 20 Februari, 2021 na kumalizika tarehe 15 Julai 2021 na kwa gharama ya shilingi bilioni 1.3 badala ya ile ya mkandarasi ya 1.9.”
Aidha, Waziri Mkuu amelitaka Jeshi la Polisi kuendelea kufuata miongozo iliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kufanya kazi kwa weledi na kuboresha mifumo ya kiutendaji wa jeshi hilo ikiwa ni pamoja na kushirikiana na vyombo vingine ili kuepuka ucheleweshwaji wa upelelezi wa kesi kwa lengo la kuondoa mlundikano wa mahabusu magerezani.
“Naliagiza Jeshi la polisi liendelee kuimarisha mfumo wa ulinzi na usalama kwenye ngazi ya jamii ili kujenga mfumo wa kutambua, kutoa taarifa na kuchukua hatua za awali dhidi ya vihatarishi vya ulinzi na usalama vinavyojitokeza katika maeneo yao.
Kadhalika, Waziri Mkuu ametoa wito kwa Taasisi nyingine za Serikali zinazotekeleza miradi ya ujenzi ziige mfano huo. “Ujenzi wa miradi kupitia mfumo wa nguvu kazi ukisimamiwa vema tena kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni zilizopo hutoa matokeo chanya.” amesema
“Nawaomba Jeshi la Polisi liendeleze ushirikiano na vyombo vya ulinzi na usalama vya nje ya nchi pamoja na taasisi mbalimbali za kimataifa (Interpol) katika kukabiliana na kupambana na matishio ya kiusalama na makosa yanayovuka mipaka hususan ugaidi, makosa ya kimtandao (cyber-crime), uharamia, utakatishaji fedha haramu, biashara haramu ya dawa za kulevya, usafirishaji haramu wa binadamu, ujangili na bidhaa bandia,”
Kwa Upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Khamis Hamza Chilo, amesema Wizara yake iko thabiti katika kusimamia Sheria na wako tayari kuhakikisha raia wote na mali zao wanaishi kwa usalama na utulivu na kutoa wito kwa watu wote wanaopanga kufanya matendo ya kiuhalifu kuacha mara moja.
Naye, Inspekta Jenerali wa Polisi, Simon Sirro amesema ujenzi huo umekamilika kwa kipindi cha miezi mitano kwa kutumia mfumo wa nguvu kazi, (Force Account) ambapo jengo hilo lina ghorofa mbili, vyumba vya ofisi 30 na kumbi mbili za mikutano.
8/30/2021
RC KUNENGE AHUZUNISHWA NA AJALI YA MOTO ILIYOTEKETEZA NYUMBA 19 HUKO RUFIJI
NA MWANDISHI WETU PWANI.
Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge amehuzunishwa na tukio la ajali ya moto uliopelekea nyumba zaidi ya 19 kuteketea kabisa kwa moto kwenye Kitongoji cha Shaurimoyo, Kijiji cha Nyamwage Wilayani Rufiji.
Ajali hiyo imetokea baada ya mwananchi mmoja aliyekuwa akisafisha shamba lake kwa kuchoma moto na moto huo kuwa mkubwa hali iliyopelekea kushindwa kuudhibiti na hivyo kuunguza nyumba.
Akizungumza kwenye eneo hilo la tukio usiku wa kuamkia leo Agosti 30, 2021 akiwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, ameagiza serikali ya wilaya kufanya tathmini kwa haraka ili kujua ukubwa wa athari iliyosababishwa na ajali hiyo na hivyo msaada unaohitajika utolewe haraka.
"Nimehuzunishwa sana na ajali hii na niwape pole wote mlioathirika na moto huu, na pia nawapongeza sana wananchi waliochukua hatua za haraka kwa kuwahifadhi na kuwasaidia wanakijiji wenzenu," alisema RC Kunenge na kuongeza.....naagiza tathmini ifanyike kwa haraka ili tujue namna ya kuwasaidia wenzetu hawa." Alisisitiza.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowele ameeleza kuwa hakuna vifo wala majeruhi kutokana na ajali hiyo, licha ya kwamba moto umetekeleza kila kitu.
Wilaya ilichukua hatua mara moja baada ya kutokea tukio hilo na kutoa rai kwa wakazi wa wilaya hiyo kuwa makini wakati wanachoma moto kwani kwa sasa ni kipindi cha upepo mkali, alisema Mkuu huyo wa wilaya.
Wananchi wa eneo hilo nao wameeleza tukio jinsi lilivyowaathiri hivyo kuomba serikali kuweza kuwasaidia kwa haraka maana hawana mahala pa kuishi.
8/29/2021
SERIKALI YAENDELEA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI KUHUSU MATUMIZI YA TIBA ASILI NCHINI.
Na WAMJW- DOM
Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeendelea na zoezi la kutoa Elimu kwa wananchi katika maeneo ya kutolea huduma za Afya juu ya umuhimu wa matumizi ya tiba asili/mbadala katika mapambano dhidi ya magonjwa mbali mbali, ikiwemo UVIKO-19.
Katika kuelekea maadhimisho ya siku ya tiba asili ya mwafrika Wadau wa tiba asili wakiongozwa na kitengo cha Tiba asili na Baraza la tiba asili kutoka wizara ya afya wameweza kutembelea na kutoa elimu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Dodoma, kituo cha Afya cha Makole na Hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma.
Akiongea wakati wa utoaji elimu hiyo Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Tiba Asili/Mbadala Dkt. Vumilia Liggie alisema kuwa, Wataalamu wa Tiba asili na tiba mbadala kutoka Wizarani wameongozana na Waganga wa tiba hizo kutembelea vituo vya Afya katika sehemu ya wagonjwa wa nje wa Hospitali (OPD) ambapo wameweza kuzungumza na wagonjwa na kuwapa elimu kuhusu umuhimu wa tiba asili katika mapambano dhidi ya magonjwa mbali mbali nchini.
"Kwa siku ya leo tumetembelea vituo vya Afya vitatu, tumetembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma General kama kituo cha kwanza, ambapo tumeenda sehemu ya wagonjwa wa nje wa Hospitali ambapo tumeweza kuzungumza na wagonjwa na kuwapa elimu kuhusu tiba asili." Alisema.
Aliendelea kusema kuwa, Serikali tuna Baraza la tiba asili na tiba mbadala ambalo linatekeleza Sheria namba 23 ya mwaka 2002 iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Baraza hili ndio linasajili dawa, Waganga wa tiba asili, na kuwajua wako wapi na wanafanya nini, na kuhakikisha dawa hizo ni salama kwa matumizi ya binadamu.
Baraza la tiba asili na tiba mbadala linafanya kazi kwa kushirikiana na Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Maabara ya TMDA, maabara ya taasisi ya dawa asili pamoja na Maabara ya Shirika la viwango Tanzania, Alisisitiza Dkt. Liggie.
Naye, Katibu Mkuu wa Shirika la dawa asilia na ulinzi wa mazingira Bw. Boniventura Mwalongo ameeleza zaidi ya asilimia 93 ya dawa zinaagizwa kutoka nje ya nchi, hivyo Serikali imelenga kuboresha tafiti za ndani, kuongeza uzalishaji wa ndani ili kutoa fursa za ajira, hususan kwa vijana, hivyo kupitia kuikuza tiba asili nchini yote yanawezekana.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Waganga wa tiba asili katika zoezi hilo Dkt. Elizabeth Lema alisema kuwa, wiki hii ya maadhimisho inatoa fursa kwa Waganga wa tiba asili na tiba mbadala kuonesha bidhaa zao mbali mbali ambazo tayari zimesajiliwa kupitia Baraza la tiba asili na tiba mbadala na kuthibitishwa kuwa ni salama kwa matumizi ya binadamu.
Aidha, ametoa rai kwa wananchi kuhudhuria maonesho hayo yatayofanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma ili kujifunza, kuelimishwa na kupata fursa ya kuuliza maswali mbali mbali kuhusu tiba asili na tiba mbadala kisha kufahamu namna ya kuzipata na kuzitumia.
Wiki ya tiba asili na tiba mbadala ya Mwafrika inaongozwa na Kauli mbiu ya "Mchango wa tiba asili katika mapambano dhidi ya UVIKO-19 " ambapo mwisho wa kilele ni Agasti 31, huku Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akitarajiwa kuwa mgeni rasmi kufunga maonesho hayo yanayofanyika kila mwaka.