MRADI WA UBORESHAJI USALAMA WA MILKI ZA ARDHI NZEGA MJINI KUKAMILIKA JUNI 30, 2024

            Na Eleuteri Mangi

Utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP)katika Halmashauri ya Mji Nzega katika mkoa wa Tabora umetekelezwa kwa asilimia 55 na kutarajiwa  kukamilika Juni 30, 2024.

Akimkaribisha Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Mhe. Japhet Hasunga  na ujumbe wake wakati wa ziara ya Kamati hiyo wilayani Nzega  tarehe 27 Machi 2024, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geophrey Pinda amesema utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi katika mji wa Nzega unatekelezwa katika mitaa 14 iliyopo Kata za Nzega Mashariki, Nzega Magharibi, Nzega ndogo, Kitangiri na Uchama.

Amebainisha kuwa, katika kata ya Nzega Mjini Mashariki mradi unatekelezwa Mitaa ya Maporomoko, Uwanja wa Ndege, Msoma, Mwaisela, Nyasa pamoja na Kitongo. Aidha, Kata ya Nzega Mjini Magharibi mradi unatekelezwa katika mitaa ya Ipilili, Mbugani, Ushirika na Utemini.

Aidha, kwa upande wa Kata ya Nzega ndogo mradi unatekelezwa kwenye mtaa wa Zogolo.  Kata ya uchama mradi unatekelezwa katika Mtaa wa Uchama na kwa kata ya Kitangiri Mradi unatekelezwa Mitaa ya Kitangiri na Budushi.

Awali akitoa taarifa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu utekelezaji wa mradi huo, Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga amesema katika halmashauri ya Mji wa Nzega mradi ulianza kutekelezwa Novemba, 2023 kwa lengo la kurasimisha vipande vya ardhi 20,000 na kuongeza Alama za Msingi za Upimaji 14.

“Hadi sasa vipande vya ardhi 18,655 vimetambuliwa, vipande 8,814 vimepangwa na viwanja 3,960 vimepimwa na Alama za Msingi za Upimaji 14 zimesimikwa ardhini, kazi hii imetekelezwa kwa asilimia 55 na bado inaendelea na itakamilika kwa wakati kama ilivyopangwa kwa kuwa sehemu kubwa kazi ambazo zinahitaji utaalam na muda mwingi zimeshakamilishwa” amesema Mhandisi Sanga.

Kwa mujibu wa Mhandisi Sanga  bajeti iliyotengwa kutekeleza Mradi huo katika Halmashauri ya Mji Nzega ni Shilingi bilioni 1.42 ambapo kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 1.396 zilitengwa kwa ajili ya urasimishaji wa makazi na Shilingi milioni 24.926 kwa ajili ya kusimika alama za msingi za upimaji.

Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Ardhi ameongeza kuwa, hadi kufikia Machi 25, 2024, jumla ya Shilingi milioni 557.779 zimetumika kutekeleza mradi huo katika Halmashauri ya Mji Nzega ambazo ni sawa na asilimia 39 ya fedha zilizotengwa.

Aidha, katika zoezi la upimaji linaloendelea, migogoro 36 imewasilishwa na migogoro 24 imetatuliwa katika kata za Nzega Mashariki, Nzega Magharibi na Kitangiri na  migogoro 12 inaendelea na hatua za utatuzi ili wananchi wapate haki ya kumiliki ardhi wanayoitumia kwa shughuli za maendeleo.

Akihitimisha ziara ya Kamati hiyo katika Halmashauri ya mji wa Nzega, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Mhe. Japhet Hasunga amesema, kazi ya Kamati hiyo ni kuangalia maendeleo ya mradi thamani ya fedha iliyotolewa na Serikali ambayo imetitishwa na Bunge kwa lengo la kutekeleza mradi huo.




Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"