DC SAME AHIMIZA UBUNIFU KATIKA UKUSANYAJI MAPATO WILAYANI HUMO
NA ASHRACK MIRAJI, SAME
Mkuu
wa Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, Mhe. Kasilda Mgeni, ameagiza Maafisa wa
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wilayani humo kutumia ubunifu, weledi pamoja
na busara katika kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi kwa baadhi ya wafanyabiashara
wasio waadilifu.
Mkuu
huyo wa Wilaya amebainisha hayo katika kikao cha Kamati ya Ushauri wa Kodi cha
Wilaya na kusisitiza kuwa mfanyabiashara yeyote atakaye bainika kuendelea
kukiuka kulipa kodi taarifa iwasilishwe Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ili hatua za
kisheria zichukuliwe dhidi yake.
Amesema
suala la ulipaji kodi ni wajibu wa kila mwananchi kisheria ili kusaidia
Serikali kupanga shughuli za kuwaletea wananchi wake maendeleo.
“TRA
fanyeni operesheni za mara kwa mara kwa wafanyabiashara wote ambao wapo ndani
ya Wilaya ya Same na wanaostahili kutumia mashine za Kielektroniki (EFD) basi
wanakuwa nazo na kwa wale ambao watakuwa wakaidi baada ya kuwafuatilia na
kuwapa elimu basi sheria iweze kuchukua mkondo wake juu yao kwani hao ni
wahujumu uchumi.” Amesisitiza
Kwa
upande wake Meneja wa TRA Wilaya ya Same, Bw. Eliapenda Mwanri, amesema
ufanisi wa utendaji unatokana na ziara
za mara kwa mara za Mkuu wa Wilaya na kamati yake ya Usalama ya kuwatembelea
Wafanyabiashara katika biashara zao kusisitiza utoaji wa risiti za
kielektroniki, ulipaji wa kodi kwa wakati pamoja na kusikiliza na kutatua kero
na changamoto za kibiashara, pia kupata
maoni ya kuboresha biashara zao.
Kwa
Mwaka wa fedha 2023/24 TRA Wilaya ya Same inakusudia kukusanya Shilingi Bilioni
4. 6 (4,637,450,937.77) sawa na ongezeko la asilimia 48% ikilinganishwa na
makusanyo ya mwaka 2022/23 ambapo lengo lilikuwa ni Shilingi bilioni 3.6 (3,
685, 320, 179.62).
Katika
kipindi cha Mwezi Julai 2023 hadi Februari 2024 imekusanya kiasi cha Shilingi
Bilioni 2.2 (2, 240, 762, 028. 53) sawa na ufanisi wa asilimia 74.2% ya lengo
la kukusanya Shilingi Bilioni 3.0 (3, 021, 651, 706. 79. na makusanyo haya sawa
na ongezeko la asilimia 8.2 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2022/23
ambayo yalikuwa Shilingi Bilioni 2.0 (2, 070, 285, 159. 60).
Comments
Post a Comment