KATAMBI: MAPITIO YA SERA YA WATU WENYE ULEMAVU YAMEANZA
Na Mwandishi Wetu, DODOMA
Serikali imeanza kufanya mapitio ya Sera ya
Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa Watu wenye Ulemavu ya Mwaka 2004 ili kukidhi
mahitaji yaliyopo.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi,
Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe.Patrobas Katambi ameyasema hayo Oktoba 31,
2023 bungeni alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti maalum (CCM),
Mhe. Stella Ikupa ambaye amehoji mkakati wa serikali kufanya marekebisho ya
Sheria namba 9 ya Mwaka 2010 ya Watu Wenye Ulemavu.
Akijibu swali hilo, Mhe.Katambi amesema mkakati
wa serikali kwa sasa ni kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma
kwa Watu wenye Ulemavu ya Mwaka 2004 ambapo utekelezaji wake umeanza.
Aidha, amesema baada ya kukamilika kwa mapitio
ya Sera ya Mwaka 2004 hatua za marekebisho ya Sheria hiyo zitaanza kwa
kuzingatia mapungufu yatakayobainishwa katika tathmini ya utekelezaji wa Sera
hiyo.
Katika swali la nyongeza, Mbunge wa Viti
maalum (CCM), Mhe.Mariam Kisangi amehoji serikali imejipangaje kutoa elimu kwa
watu wenye ulemavu ili kutoa maoni kwenye mapitio hayo.
Mhe.Katambi akijibu swali hilo, amesema
mapitio ya sera yanatarajiwa kukamilika Mwaka huu na yamekuwa shirikishi kwa
makundi yote ya watu wenye ulemavu.
Comments
Post a Comment