KWA MARA YA KWANZA MATIBABU YA UZIBUAJI WA MISHIPA YA DAMU YA MIGUU YAFANYIKA NCHINI

 

Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam

Kwa mara ya kwanza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imefanya upasuaji wa kuzibua mishipa ya damu ya miguu iliyoziba kwa wagonjwa 100 wenye matatizo hayo kwa kutumia mtambo wa Cathlab kuzibua mishipa hiyo.

Matibabu hayo yamefanyika katika kambi maalumu ya matibabu ya siku tano inafanywa na madaktari bingwa wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na  mwenzao kutoka Hospitali ya BLK iliyopo nchini India.

Akizungumzia kuhusu kambi hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema hadi leo tayari wagonjwa 40 wameshapatiwa matibabu na hali zao kuendelea vizuri ambapo baadhi ya wagonjwa tayari wameruhusiwa.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa moyo na mishipa ya damu alisema matatizo ya mishipa ya damu ya miguu kuziba yapo kwa wingi katika jamii na mara nyingi huwapata wagonjwa wa kisukari, wagonjwa wa shinikizo la juu la damu pamoja na watu wanaovuta sana sigara na kunywa sana pombe.

“Wagonjwa wengi wenye matatizo ya mishipa ya damu ya miguu kuziba wamekuwa wakikatwa miguu kwa kuchelewa kupata matibabu ama wengine kutokujua tatizo linalowasumbua hivyo kufikia hatua ya kukatwa miguu”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema JKCI imeona tatizo la mishipa ya damu ya miguu kuziba linaongezeka kwa kasi hivyo kuamua kuanzisha huduma ya matibabu hayo na kuifanya endelevu kusaidia wagonjwa wanaosumbuliwa na matatizo hayo.

“Baada ya kambi hii madaktari wetu wataendelea kutoa huduma ya matibabu ya mishipa ya miguu baada ya kupata ujuzi kutoka kwa wenzetu wa hospitali ya BLK iliyopo nchini India”, alisema Dkt. Kisenge

Aidha Dkt. Kisenge alisema JKCI inaenda kuanzisha huduma nyingine mpya kwa kushirikiana na mabingwa wa Hospitali ya BLK iliyopo nchini India ya kuzibua mishipa ya damu iliyoziba na kusababisha matatizo ya nguvu za kiume kupungua ili kuwasaidia wagonjwa wanaosumbuliwa na matatizo ya nguvu za kiume.

Kwa upande wake daktari bingwa wa moyo na mishipa ya damu kutoka Hospitali ya BLK iliyopo nchini India Suhail Bukhari alisema hii ni mara ya kwanza wataalamu kutoka Hospitali ya BLK kutoa huduma katika Taasisi hiyo lengo likiwa ni kutoa ujuzi kwa wataalam wa JKCI pamoja na kuwasaidia wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya miguuni kuziba.

Dkt. Suhail alisema upasuaji wa kuzibua mishipa ya damu ya miguu iliyoziba unafanyika kwa utaalamu wa kisasa hivyo kuwasaidia wagonjwa kuondokana na maumivu na changamoto walizokuwa wakipita.

“Nimeongea na Mkurugenzi wa JKCI na kumshauri kuwa na idara tofauti za upasuaji wa mishipa ya damu ili kusaidia wagonjwa wenye mishipa ya damu ya miguu kuziba kupata huduma kwa haraka na kufanya matibabu haya kujulikana Afrika yote”, alisema Dkt. Suhail.

Naye Daktari bingwa wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. George Longopa alisema mwamko wa wagonjwa kupata huduma katika kambi hiyo umekuwa mkubwa tofauti na ilivyotarajiwa hivyo kuonyesha kuwa tatizo la mishipa ya damu ya miguuni kuziba kuwa kubwa.

“Tulipotoa tangazo kuhusu matibabu haya wagonjwa zaidi ya 200 walijitokeza hivyo kuwagawanya katika makundi na kuanza na wagonjwa 100 katika kambi hii, wagonjwa wengine waliobaki tutaendelea kuwahudumia kwani tayari tumeshapata ujuzi”, alisema Dkt. Longopa.

Dkt. Longopa alisema wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya miguuni kuziba sasa watakuwa wanapatiwa matibabu JKCI na wale ambao watakuwa na matatizo makubwa zaidi wataendelea kushirikiana na wataalam wa afya kutoka Hospitali ya BLK iliyopo nchini India ili ujuzi uzidi kukuwa na kupunguza idadi ya wagonjwa wanaokwenda nje ya nchi kwaajili ya matibabu.

Naye Betha Mkwawa aliyepata matibabu katika kambi hiyo alisema amesumbuliwa na maumivu ya miguu kwa muda wa miaka zaidi ya kumi bila kujua kama mishipa yake ya damu kwenye miguu imeziba.

Betha alisema baada ya kupata ajali na kuvunjika mguu alipatiwa matibabu nchini India miaka 13 iliyopita na baada ya matibabu hayo alianza kuumwa mguu lakini kila alipoenda hospitali kutibiwa aliambiwa maumivu anayoyapata yanatokana na ajali aliyoipata.

“Nimehangaika sana na huu mguu hadi mwaka 2017 nilipogundulika kuwa mishipa yangu ya damu ya miguu imeziba haiwezi kupitisha damu vizuri nikaanzishiwa dawa hadi mwaka huu nilipoona tangazo la matibabu ya mishipa ya damu ya miguu kuziba nikaona ni wakati sasa wa kufika hapa JKCI na kutibiwa”,

“Namshukuru Mungu nimepata matibabu na baada ya matibabu tu nimeona mabadiliko kwani sasa mguu wangu umekuwa mwepesi, maumivu hakuna, hali ya kuvimba imeondoka sasa mguu umenywea naamini na hii hali ya mguu kuwa mweusi inaenda kuisha”, alisema Betha.





Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"