GAVANA TUTUBA: SHILINGI YA TANZANIA IMEENDELEA KUIMARIKA

NA HUGHES DUGILO, DAR ES SALAAM.

GAVANA wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Bw. Emmanuel Tutuba ameseSma hilingi ya Tanzania kwa muda mrefu imeendelea kuwa imara ikilinganishwa na sarafu nyingine kwenye ukanda wa Afrika Mashariki. Gavana Tutuba ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari alipofanya ziara ya kutembela Banda la BoT katika Maonesho ya Biashara ya 47 ya Kimataifa ya Dar es Salaam maarufu Sabasaba yanayoendelea kwenye Viwanja vya Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam. Amesema tathimini imeonyesha kuwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita Shilingi ya Tanzania imeshuka thamani kwa asilimia 1.4 tu, ambapo ni sarafu chache sana Ulimwenguni zenye uhimilivu kama ilivyo sarafu ya Tanzania. “Kinachofanya Shilingi yetu kuwa himilivu ni sababu ya vyanzo vya shughuli za uzalishaji, unajua uhimilivu wa shilingi unategemea na aina ya biashara na huduma ambazo zinaenda kufanya mzunguko wa fedha. “Kwa muda mrefu thamani ya Shilingi yetu imeendelea kuwa imara kwa sababu pia hata mfumuko wa bei haujawa mkubwa sana, na inatokana na Sera madhubuti za fedha,” alidokeza Gavana Tutuba na kuongeza..kama Benki Kuu tumeendelea kusimamia eneo la Sera za fedha ambazo tunatoa mwelekeo wake mara kwa mara kwenye tovuti yetu.’ Alifafanua. Aidha ameongeza kuwa muelekeo wa uchumi ni kuhakikisha uchumi wa nchi unazidi kuimarika na kupunguza mfumuko wa bei ambapo lengo lilikuwa asilimia 5 katika kipindi cha muda wa kati. “Kwa kulisimamia hili inatufanya tunapotoa fedha kuingia kwenye mzunguko wa uchumi tunakuwa tunaufuatilia, unajua kwenye mzunguko wa fedha, fedha zote huwa ziko Serikalini, kwa hiyo zinapotoka huwa tunazipeleka kwenye Taasisi mbalimbali au kuzipeleka kwa wananchi, utaona Serikali inalipa mishahara au imetekeleza miradi mbalimbali ikimlipa mkandarasi, maana yake Serikali imetoa fedha kwenda kwa Wananchi,”ametabanaisha Gavana huyo wa Benki Kuu ya Tanzania. 

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Bw. Emmanuel Tutuba akipata maelezo kutoka kwa Afisa Mwandamizi Mkuu Usimamizi wa Safaru wa Benki hiyo  Bi. Crispina Nkya (wa kwanza kulia), kuhusu njia mbalimbali zinazotumika kutambua noti feki  wakati alipotembelea Katika Banda la Benki hiyo, kwenye maonesho ya Biashara ya 47 ya Kimataifa (Sabasaba) yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam. (wa pili kulia), ni Mhasibu Mkuu Mwandamizi BoT, Elirehema Msemembo.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Bw. Emmanuel Tutuba (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mchambuzi wa Mifumo ya Malipo Benki hiyo Nestory Maro (wa kwanza kulia), kuhusu uendeshaji na Usimamizi wa Mifumo ya Malipo, inayosimamiwa na Kurugenzi ya Mifumo ya Malipo ya Taifa.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Bw. Emmanuel Tutuba (kushoto), akitoa maelekezo kwa Afisa Mwandamizi wa BoT, anayeshughulikia Huduma ndogo za fedha Bi. Mwile Kauzeni (kulia) alipokuwa kwenye ziara ya kutembelea Banda la Benki hiyo katika Maonesho ya Biashara ya 47 ya Kimataifa, (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam. (PICHA NA: HUGHES DUGILO).

Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"