WANACHUO WA CHUO CHA UHASIBU, IAA JIJINI ARUSHA WACHANGAMKIA "BOOM VIBES NA NSSF" KWA KUJIUNGA NA MFUKO

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, ARUSHA

KAMPENI ya “BOOM VIBES NA NSSF” yenye lengo la kuhamasisha Wanachuo kuhusu Hifadhi ya Jamii na Uwekaji Akiba imefanyika kwenye Chuo cha Uhasibu jijini Arusha (IAA) leo Mei 31, 2022.

Kampeni hiyo ni mkakati wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) chini ya Mpango wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa sekta isiyo rasmi kutembelea taasisi mbalimbali za elimu ya juu na kati nchini ili kuhamasisha wanachuo kujenga tabia ya kujiwekea akiba kwa kujiunga na Mfuko na kuchangia kila mwezi ili hatimaye wanufaike na mpango wenyewe, Meneja wa Sekta Isiyo Rasmi, NSSF Bi. Rehema Chuma amewaambia wanachuo hao wakati akitoa  Elimu ya Hifadhi ya Jamii.

Alisema wanachuo ni wanufaika wakubwa wa mpango huo kutokana na kipato wanachokipata wanaweza kutenga ziada na kujiwekea akiba NSSF kwa manufaa ya sasa na baadaye.

“Ni muhimu wewe kama mwanachuo kuwa na utamaduni wa kujiwekea akiba kupitia NSSF, ukianza kuweka akiba mapema itakuwezesha kuwa na akiba ya kutosha kwa faida ya sasa na baadaye.” Alisisitiza.

Kuhusu namna ya kuchangia, Meneja huyo alifafanua kuwa mwanachama wa NSSF anatakiwa kuhakikisha anachangia kiasi kisichopungua shilingi elfu ishirini (20,000/=) kila mwezi au zaidi.

“Uwasilishaji wa michango ya kila mwezi ni rahisi sana unaweza kufanya hivyo kupitia simu yako ya mkononi ukiwa popote pale, lakini pia unaweza kuwasilisha kupitia benki au mawakala wa benki.” Alifafanua.

Katika kuunga mkono mkakati huo wa NSSF, baadhi ya Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria na Katiba, Mhe.Suma Fyandomo,Mhe.Joseph Tadayo na Mhe. Agnes Hokororo wameshiriki katika kampeni hiyo ambapo wamesisitiza umuhimu wa wanachuo kuchangamkia fursa hiyo kwa kujiunga na Mfuko na kujiwekea akiba.

Mwanachuo wa Chuo Cha Uhasibu Arusha (IAA), akijaza fomu ya kujiunga na NSSF baada ya kupatiwa elimu ya Hifadhi ya Jamii na Kuweka akiba kwenye ukumbi wa chuo Mei 31, 2022.
Wanachuo wakionyesha fomu za kujiunga na NSSF baada ya kuzijaza.
Meneja wa Sekta Isiyo Rasmi, NSSF Bi. Rehema Chuma Akitoa elimu ya Hifadhi ya Jamii na kuweka akiba kwa wanachuo wa IAA.
Mhe. Suma Fyandomo; “Niwasihi sana, pesa mnayopata kila mwezi iwe ni kutoka kwenye mkopo au kwa wazazi, msiitumie yote kwenye matumizi yenu, mnaweza kuanza kuweka akiba kupitia NSSF na mkianza kuweka akiba kuanzia sasa, itakapofika muda wa kumaliza elimu yenu akiba mliyoweka inaweza kuwasaidia katika maisha yenu hapo baadaye na hamtajutia uamuzi wenu.” Alisisitiza Mhe. Suma Fyandomo ambaye licha ya kuwa Mbunge, pia ni mjasiriamali.

Mhe. Joseph Tadayo; “Nilijiunga na NSSF na kuanza kuchangia  kabla sijawa mbunge, miaka hiyo ya nyuma ya umri wangu huduma nyingi zilikuwa bure na hata ajira pia zilikuwa tele, kwa sasa hali haiku hivyo mtu anakuwa nacho sio kwa kile anachoingiza bali kile anachoweka, tunahitaji kuwa na utamaduni wa kuweka akiba tena kutokana na kile ulichovuna kutokana na jasho lako.” Mhe. Tadayo.

"Niliwahi kuuza mayai ya kuchemsha, nimeuza mifuko ya kubebea bidhaa, lakini pia nimefanya kazi ya uhudumu kwenye mgahawa na hata nilipokuwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nilikuwa nafundisha masomo ya ziada “tuition” na ninyi mnaweza kujiwekea akiba kupitia pato unalopata hapa chuoni la mkopo na wengine fedha za kujikimu kutoka kwa wazazi, lazima tuweke akiba ili kukabiliana na maisha yetu hapo baadaye.” Mhe. Tadayo.

Mhe. Agnes Hokororo; “Vijana mnapaswa kuelekeza fikra zenu katika kujiajiri baada ya kuhitimu elimu yenu, ninyi mmepata bahati ya kuelimishwa kujiwekea akiba chini ya kampeni ya Boom Vibes na NSSF, changamkieni fursa hii kwani hamtajutia uamuzi wenu, kwa hakika naichukulia kama vile mmekutana na gari la mshahara, msikubali mpishane nalo." Aliwasisitizia.

Meneja wa NSSF jijini Arusha, Bw.Josephat Komba.
Mwakilishi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Festo Fute, akizungumza.


Wanafunzi wakijaza fomu za kujiunga na NSSF
Wanafunzi wakijaza fomu za kujiunga na NSSF
Meneja wa Sekta Isiyo Rasmi, NSSF Bi. Rehema Chuma(kushoto), alibadilishana mawazo na Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma, Bi. Lulu Mengele
Wanafunzi wakijaza fomu za kujiunga na NSSF.
Bi. Halima Juma Malole, Afisa Matekelezo NSSF Mkoani Arusha, akimpiga picha ya kitambulisho mwanachuo wa IAA baada ya kujaza fomu.

Bi. Halima Juma Malole, Afisa Matekelezo NSSF Mkoani Arusha, akitoa ufafanuzi kwa wanachuo wakati zoezi la kujaza fomu za kujiunga na Mfuko likiendelea.

Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"