WAKILI MKUU WA SERIKALI AWAPONGEZA WAFANYAKAZI KWA MAFANIKIO MAKUBWA YALIYOPATIKANA NDANI YA MUDA MFUPI

NA DENNIS BUYEKWA – MOROGORO

SERIKALI ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mh. Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na watumishi wa Umma wakiwemo watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali katika kuiletea maendeleo nchi yetu.

Hayo yamezungumzwa mapema leo na Wakili Mkuu wa Serikali Bw. Gabriel Pascal Malata wakati akifungua kikao cha tatu cha Baraza la wafanyakazi wa ofisi hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) uliopo mkoani Morogoro.

Bw. Malata amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo mwaka 2018, ofisi yake imeendelea kutekeleza vyema majukumu yake ya Uratibu, Usimamizi, Ushauri, na Uendeshaji wa Mashauri yote ya Madai na Usuluhishi yanayofunguliwa dhidi ya Serikali pamoja na Taasisi zake ndani na nje ya nchi.

Ameongeza kuwa ili tuweze kufikia malengo ya vipaumbele vikubwa katika nchi yetu ambavyo vimewezesha kuifanya Tanzania kuwa Nchi ya Uchumi wa kati, kuvutia wawekezaji na ujenzi wa viwanda, ni muhimu kuwa na uwazi na ushirikishwaji baina ya viongozi katika taasisi mbalimbali za umma pamoja na watendaji ambao ni watumishi wa ngazi zote wanaozingatia sheria, taratibu, na miongozo mbalimbali ya nchi.

naomba nitoe wito kwa wajumbe na washiriki wote wa Baraza hili kutumia fursa hii mliyoipata kuhoji na kutoa mapendekezo chanya yatakayokuwa na msaada kwa taasisi yenu ili hatimaye mchango wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali uonekane katika jitihada za pamoja za kuiletea maendeleo nchi yetu”, alisema Bw.Malata

Akizungumza kuhusu mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo, Bw. Malata amesema kuwa ofisi yake imefanikiwa kuokoa shilingi za kitanzania Trioni 11.4 baada ya kushinda mashuri mbalimbali yaliyofunguliwa dhidi ya serikali kiasi ambacho kingelipwa kama Serikali ingeshindwa katika mashauri hayo.

Ameongeza kuwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali CAG) kwa mwaka wa fedha 2018/2019 inaonyesha kuwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imepata hati safi katika taarifa ya hesabu zake za fedha katika kipindi hicho ikiwa ni mwaka mmoja tu tangu kuanzishwa kwake.

Hati safi ya ukaguzi wa taarifa ya fedha ni uthibitisho kuwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ina udhibiti bora katika kusimamia rasilimali za serikali”, alisema Bw. Malata.

Aidha kutokana na mafanikio ambayo nchi yetu imekuwa ikiyapata katika nyanja mbalimbali ikiwemo nyanja ya kiuchumi, baadhi ya watu wasiotutakia mema wamekuwa wakijaribu kufanya hujuma ili kuharibu na kuturudisha nyuma katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo aidha kwa maslahi yao binafsi au kwa maslahi ya watu wanaowatuma.

Akielezea kuhusu hatua zilizochukuliwa dhidi ya watu hao wenye nia mbaya, kwa mamlaka na wajibu ilionao, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali daima imeiwakilisha Serikali vyema katika Mahakama mbalimbali ndani na nje ya nchi katika kudai na kutetea haki hatua iliyopelekea kuokoa mali za serikali ambazo zingepotelea mikoni mwa watu hao wenye nia ovu.

Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali pia  imefanikiwa kuboresha maktaba yake kwa kununua vitabu vya sheria,  nakala za sheria na machapisho mbalimbali hatua ambayo imesaidia kuwaongezea ujuzi watumishi wake hasa wanasheria hatua ambayo imeisaidia serikali kushinda mashauri mengi yanayofunguliwa dhidi yake.

Kuhusu uboreshwaji wa miundombinu ya ofisi wakili Mkuu wa Serikali amesema kuwa ofisi yake imefanikiwa kuweka mifumo ya kielektroniki ya kusajili, kuendesha, kusambaza na kusimamia mashauri kwa mawakili na watumishi mbalimbali, ikiwemo mfumo wa uendeshaji wa mashauri ndani na nje kwa njia ya kielekroniki (Video Conference) hatua iliyosaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri kwani mawakili hawalazimiki kusafiri kwenda katika mikoa mbalimbali kuendesha mashauri badala yake wamekuwa wakisimamia mashauri hayo wakiwa ofisini hapo.

Bw. Malata amewapongeza wajumbe wa Sekretariat kwa  maandalizi mazuri waliyofanya  katika kuhakikisha  kikao hicho kinafanyika huku akiwakumbusha wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, kujadili masuala yote yatakayoletwa mbele yenu kwa weledi, hekima na busara ili Baraza hili liwe na tija ofisi na taifa kwa ujumla. Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kimefanyika baada ya mafunzo ya siku moja kuhusu umuhimu wa vyama vya wafanyakazi na wajibu wa wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi.

Wakili Mkuu wa Serikali Bw. Gabriel Malata akisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari pamoja na Wajumbe waliohudhuria kikao hicho mapema leo mkoani Morogoro.

Baadhi ya Wajumbe waliohudhuria kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika kikao hicho.


 

Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"