WAHANDISI 264 WACHUKULIWA HATUA KUKIUKA MAADILI
NA MWANDISHI WETU, DODOMA
BODI ya Usajili wa Wahandisi (ERB), imesema kuwa
imechukua hatua kwa wahandisi 264 katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka
2015 hadi 2020 kutokana na makosa mbalimbali ya ukiukwaji wa maadili ya taaluma
ya kiuhandisi ambayo ni kinyume na kiapo chao.
Hayo yamesemwa na Msajili wa Bodi hiyo Mhandisi
Patrick Barozi, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, kuhusiana
na maadhimisho ya Siku ya Wahandisi kwa mwaka huu ambayo yatafanyika jijini
humo tarehe 3 na 4 mwezi Septemba.
Mhandisi Barozi, amefafanua kuwa hatua hiyo
huchukuliwa na bodi hiyo mara tu baada
ya wahandisi hao kula kiapo cha utii ambacho kinawakumbusha kuwajibika vyema kwenye
taaluma zao na maamuzi yao ya utendaji wao wa kihandisi wa kila siku.
“Bodi imechukua hatua mbalimbali kwa wahandisi 264 ikwemo kuwaonya na
kuwapeleka mahakamani wahandisi ambao walionekana kukiuka kiapo chao cha utii
katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, na itaendelea kufuatilia wahandisi
ambao hawana maadili lengo ni kuhakikisha wahandisi wanazingatia maadili ya
taaluma yao siku zote”, amefafanua Barozi.
Kuhusiana na siku hiyo ya wahandisi Mhandisi Barozi
amesisitiza kuwa mbali na kuwa na shughuli mbalimbali zitakazofanywa, pia
wataalamu watakula kiapo cha utii kama ilivyo kwa miaka mingine ili kufanya
wawajibike vyema kwenye taaluma zao.
Aidha, ametaja shughuli nyingine zitakazofanyika ni
pamoja na kuwepo kwaa kongamano la wahandisi vijana, majadiliano ya kitaaluma,
maonesho mbalimbali ya ubunifu na teknolojia na biashara, kutoa tuzo mbalimbali
kwa awahandisi na makampuni , kuwatambua na kuwazawadia wahandisi wahitimu
waliofanya vizuri katika mitihani yao ya mwaka wa mwisho wa 2019/2020.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya maadhimisho ya
Siku ya Wahandisi, Profesa Bakari
Mwinyiwiwa amesema kuwa lengo kuadhimisha siku ya wahandisi ni kuuwezesha umma
kutambua michango chanya inayofanywa na wahandisi wa Tanzania katika maendeleo
ya kijamii na kiuchumi nchini.
Ametanabaisha kuwa lego jingine ni kuwatambua
wahandisi hao, makampuni na mashirika ya kihandisi yaliyotoa michango mikubwa
ya kihandisi katika maendeleo ya Taifa na hivyo kuwahamasisha wahandisi wengine
kufanya shughuli zao vizuri zaidi.
Maadhimisho ya Siku ya wahandisi Tanzania kwa mwaka huu
ambayo yanafanyika kwa mara ya 17 tangu kuanzishwa kwake yanatarajiwa
kushirikisha wahandisi zaidi ya 5000 kutoka sehemu mbalimbali ikiwemo Zimbabwe,
Kenya, Nigeria, Uganda, Rwanda, Misri, Malawi, Botswana na Kenya.
Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya maadimisho ya Siku ya Wahandisi kwa
mwaka huu, Profesa Bakari Mwinyiwiwa, akisisitiza jambo wakati uongozi wa bodi
hiyo ulipokutana na waandishi wa habari kuzungumzia kuhusu maadhimisho ya siku
hizo yanayotarajiwa kufanyika tarehe 3 na 4 mwezi
Septemba, 2020 jijini Dodoma.
Msajili wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi, Mhandisi Patrick Barozi, akifafanua jambo wakati uongozi wa bodi hiyo ulipokutana na waandishi wa habari kuzungumzia kuhusu maadhimisho ya Siku ya Wahandisi yanayotarajiwa kufanyika tarehe 3 na 4 mwezi Septemba, 2020 jijini Dodoma.
Comments
Post a Comment