WALIMU WA HEDHI RUKWA WAJA NA MUAROBAINI WA TAULO ZA KIKE

Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Rukwa Winnie Kijazi akitoa nasaha wakati wa kufungua mafunzo ya Hedhi Salama kwa baadhi ya waalimu wa Shule za Msingi Mkoani Rukwa.

 

Baadhi ya Waalimu kutoka halmashauri ya wilaya ya Kalambo wakionesha vyeti vyao baada ya kupatiwa mafunzo ya Hedhi Salama wakiwa katika picha ya pamoja na Mratibu wa Mradi wa SWASH Mkoa Matinda Mwinuka (aliyechuchumaa kushoto) na Mwezeshaji Jesca Lwiza (aliyechuchumaa kulia)

 NA MWANDISHI WETU, RUKWA

UMOJA wa Walimu wa Hedhi Salama kwa shule za msingi mkoani Rukwa wamepania kuhakikisha wanapunguza fikra potofu kuhusu suala la hedhi kwa wasichana wanaovunja ungo pamoja na kukomesha utoro kwa wananfunzi wa kike wanaoona aibu kuhudhuria shule pindi wanapopata hedhi kwa kutoa elimu sahihi ya suala la hedhi mashuleni.

Azma hiyo imekuja baada ya waalimu hao kupewa mafunzo yanayohusu namna ya kutengeneza taulo za kike (pedi) kwa kutumia aina mbalimbali za vitambaa pamoja na kukabiliana na wanafunzi wanaoona aibu ama fedheha pindi wanapopata hedhi wakiwa shuleni na hivyo kuwarahisishia Maisha yao wanapokuwa shuleni huku wakiwahamasisha kuendelea kuhudhuria shuleni ili wasiachwe nyuma kimasomo.

Aida Mwanauta ni mwalimu wa Hedhi Salama kutoka Shule ya Msingi Ilambila, Wilayani Kalambo, aliishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo hayo muhimu kwani changamoto wanazokumbana nazo ni nyingi na mafunzo hayo yamamsaidia kujua namna ya kuwasaidia wasichana hao pindi wanapokuwa katika hedhi kutokana na wanafunzi wengi kutokuwa na ufahamu wa kutosha juu ya namna ya kukabilina na hali hiyo.

“Kuna mwanafunzi anakuja shuleni hajui ni namna gani anaweza akajistiri, mwingine anatoka nje anakimbia, huko nje anachukua hata makaratasi, majani kwaajili ya kujistiri ambayo inaweza ikamletea matatizo baadaye, kwahiyo katika semina hii tumejifunza mambo mbalimbali, tumejua ni mambo gani ambayo unaweza ukamfundisha mtoto, akajua jinsi ya kujihifadhi akiwa shuleni na hatimae akawa anasoma na asiwe mtoro shuleni, na kujiona ni sawa na wengine,” Alisema.

Nae, Mwalimu Victoria Tanganyika alisema kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kujua vifaa vinavyotumika kutengeneza pedi za kike na namna ya kuvitekeza pamoja na kujua mazungumzo anayotakiwa kufanya na matoto ili kumshawishi aweze kujiamini  na kushiriki katika michezo na masomo katika mazingira ya shule.

Kwa upande wake Mwalimu Clifonsia Remidio ameiomba serikali kuendelea kutumia njia mbalimbali za vipeperushi na kutoa semina kwa waalimu wengi zaidi wanaotoa huduma ya hedhi salama mashuleni ili kuweza kuwasaidia wanafunzi wa kike ambao wamekuwa wakipata tabu kusoma wanapokuwa katika kipindi cha hedhi.

“kuna vitu vingi tulikuwa hatuvifahamu, kuna wakati mwingine hata kama mimi mwalimu nimeshasoma lakini bado nitaona aibu kuenenda kumuelekeza yule mwanafunzi, lakini ameshatuelekeza mwezeshaji tumepata mwanga mzuri pia nimefurahi kwasababu hili suala linashirikisha pande zote mbili, upande wa waalimu wa kiume na upande wa waalimu wa kike pia kwamba tuwasaidie Watoto wanaposikia ile hali ya mabadiliko ya mwili,”Alisema.

Aidha, Mwezeshaji wa mafunzo hayo ya Hedhi Salama, Mwalimu Jesca Lwiza alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kutoa elimu ya hedhi salama kwa wanafunzi ili kupunguza utoro mashuleni na kuongeza kuwa wanategemea kuona mabadiliko makubwa ya mahudhurio shule kwa shule ambazo waalimu wake wamehudhuria mafunzo hayo.

“Kuna ukimya ambao upo katika masuala ya hedhi salama, wanafunzi wanakosa elimu sahihi, lakini pia wanakosa namna ya kujiamini wanapokuwa katika masomo na wakati mwingine shuleni hakuna vyumba maalum vya kujihifadhi wanapokuwa katika hedhi, kwa kulitambua hilo tumeona serikali namna ilivyoweza kuwezesha kwa kuwapa mafunzo waalimu lakini imeweza kuboresha miundombinu iliyopo mashuleni kwa kuweka vyumba hivyo,” Alisema.

Wakati akifungua mafunzo hayo Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Rukwa Winnie Kijazi alisisitiza kuwa tafiti zilizofanyika zimeonesha kuwa wasichana wengi hawana taarifa za awali kuhusu hedhi za pia walipata hedhi ya kwanza pasipo kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu mabadiliko ya miili yao hivyo mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo waalimu kufikisha elimu katika shule.

“Tafiti zinaonesha kuwa bado kuna fikra zisizo sahihi kuhusu masuala ya hedhi hususani miiko na unyanyapaa inayosababisha wasichana na wanawake kushindwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kijamii na wanafunzi wa kike kukosa baadhi ya siku za masomo na wengine kuacha shule wanapokuwa kwenye hedhi. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kulitambua hilo imeweka jitihada kuhakikisha kuwa fursa za elimu zinapatikana kwa makundi yote,” Alieleza.

Halikadhalika mratibu wa mradi wa School Water Sanitation and Hygiene (SWASH) Mwalimu Matinda Mwinuka aliwaasa waalimu kuhakikisha shule zinakuwa na vyombo maalum kwaajili ya walemavu pamoja na vyumba kwaajili ya wasichana kubadili pedi za hedhi pindi wanapokuwa katika hali hiyo nasio kutumia vyoo vya kawaida ambavyo havina mazingira mazuri ya kubadilishia vifaa vyao.

“Kuna shule moja fundi kaweka shule maalum, anasema kuwa kile ndio chumba maalum, walemavu wataingia humo humo, hedhi salama wataingia humo humo, ametoboa tundu na kuweka ‘pipe’ anasema Watoto wa kike wakishaingia humu ndimo watatumbukiza vile vitu vyao yaani ni vitu vya ajabu kwakweli.”

Mradi huo unatekelezwa katika halmashauri tatu za Mkoa wa Rukwa kwa muda wa miaka minne huku kwa mwaka wa fedha 2019/2020 Mkoa ulipewa kiasi cha Shilingi 578,486,955.63/= kwaajili ya utekelezaji wa mradi huo unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na kutekelezwa katika mikoa 17 na Halmashauri 86 za Tanzania Bara ukiwa na lengo la kuboresha mazingira ya kufundishia, kujenga vyoo bora shuleni na kuweka miundombinu ya maji safi na salama.

 


Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"