WALIMU WA HEDHI RUKWA WAJA NA MUAROBAINI WA TAULO ZA KIKE
Kaimu Katibu
Tawala Mkoa wa Rukwa Winnie Kijazi akitoa nasaha wakati wa kufungua mafunzo ya
Hedhi Salama kwa baadhi ya waalimu wa Shule za Msingi Mkoani Rukwa.
Baadhi ya
Waalimu kutoka halmashauri ya wilaya ya Kalambo wakionesha vyeti vyao
baada ya kupatiwa mafunzo ya Hedhi Salama wakiwa katika picha ya pamoja na
Mratibu wa Mradi wa SWASH Mkoa Matinda Mwinuka (aliyechuchumaa kushoto) na
Mwezeshaji Jesca Lwiza (aliyechuchumaa kulia)
NA MWANDISHI WETU, RUKWA
UMOJA wa Walimu
wa Hedhi Salama kwa shule za msingi mkoani Rukwa wamepania kuhakikisha
wanapunguza fikra potofu kuhusu suala la hedhi kwa wasichana wanaovunja ungo
pamoja na kukomesha utoro kwa wananfunzi wa kike wanaoona aibu kuhudhuria shule
pindi wanapopata hedhi kwa kutoa elimu sahihi ya suala la hedhi mashuleni.
Azma hiyo imekuja baada ya waalimu hao kupewa mafunzo yanayohusu
namna ya kutengeneza taulo za kike (pedi) kwa kutumia aina mbalimbali za vitambaa pamoja na
kukabiliana na wanafunzi wanaoona aibu ama fedheha pindi wanapopata hedhi
wakiwa shuleni na hivyo kuwarahisishia Maisha yao wanapokuwa shuleni huku
wakiwahamasisha kuendelea kuhudhuria shuleni ili wasiachwe nyuma kimasomo.
Aida Mwanauta ni mwalimu wa Hedhi Salama kutoka Shule ya Msingi
Ilambila, Wilayani Kalambo, aliishukuru serikali kwa kuwapatia mafunzo hayo
muhimu kwani changamoto wanazokumbana nazo ni nyingi na mafunzo hayo
yamamsaidia kujua namna ya kuwasaidia wasichana hao pindi wanapokuwa katika
hedhi kutokana na wanafunzi wengi kutokuwa na ufahamu wa kutosha juu ya namna
ya kukabilina na hali hiyo.
“Kuna mwanafunzi anakuja shuleni hajui ni namna gani anaweza
akajistiri, mwingine anatoka nje anakimbia, huko nje anachukua hata makaratasi,
majani kwaajili ya kujistiri ambayo inaweza ikamletea matatizo baadaye, kwahiyo
katika semina hii tumejifunza mambo mbalimbali, tumejua ni mambo gani ambayo
unaweza ukamfundisha mtoto, akajua jinsi ya kujihifadhi akiwa shuleni na
hatimae akawa anasoma na asiwe mtoro shuleni, na kujiona ni sawa na wengine,”
Alisema.
Nae, Mwalimu Victoria Tanganyika alisema kuwa mafunzo hayo
yamemsaidia kujua vifaa vinavyotumika kutengeneza pedi za kike na namna ya
kuvitekeza pamoja na kujua mazungumzo anayotakiwa kufanya na matoto ili
kumshawishi aweze kujiamini na kushiriki katika michezo na masomo katika
mazingira ya shule.
Kwa upande wake Mwalimu Clifonsia Remidio ameiomba serikali
kuendelea kutumia njia mbalimbali za vipeperushi na kutoa semina kwa waalimu
wengi zaidi wanaotoa huduma ya hedhi salama mashuleni ili kuweza kuwasaidia
wanafunzi wa kike ambao wamekuwa wakipata tabu kusoma wanapokuwa katika kipindi
cha hedhi.
“kuna vitu vingi tulikuwa hatuvifahamu, kuna wakati mwingine
hata kama mimi mwalimu nimeshasoma lakini bado nitaona aibu kuenenda
kumuelekeza yule mwanafunzi, lakini ameshatuelekeza mwezeshaji tumepata mwanga
mzuri pia nimefurahi kwasababu hili suala linashirikisha pande zote mbili, upande
wa waalimu wa kiume na upande wa waalimu wa kike pia kwamba tuwasaidie Watoto
wanaposikia ile hali ya mabadiliko ya mwili,”Alisema.
Aidha, Mwezeshaji wa mafunzo hayo ya Hedhi Salama, Mwalimu Jesca
Lwiza alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kutoa elimu ya hedhi salama kwa
wanafunzi ili kupunguza utoro mashuleni na kuongeza kuwa wanategemea kuona
mabadiliko makubwa ya mahudhurio shule kwa shule ambazo waalimu wake
wamehudhuria mafunzo hayo.
“Kuna ukimya ambao upo katika masuala ya hedhi salama, wanafunzi
wanakosa elimu sahihi, lakini pia wanakosa namna ya kujiamini wanapokuwa katika
masomo na wakati mwingine shuleni hakuna vyumba maalum vya kujihifadhi
wanapokuwa katika hedhi, kwa kulitambua hilo tumeona serikali namna ilivyoweza
kuwezesha kwa kuwapa mafunzo waalimu lakini imeweza kuboresha miundombinu
iliyopo mashuleni kwa kuweka vyumba hivyo,” Alisema.
Wakati akifungua mafunzo hayo Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Rukwa
Winnie Kijazi alisisitiza kuwa tafiti zilizofanyika zimeonesha kuwa wasichana
wengi hawana taarifa za awali kuhusu hedhi za pia walipata hedhi ya kwanza
pasipo kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu mabadiliko ya miili yao hivyo mafunzo
hayo yamelenga kuwajengea uwezo waalimu kufikisha elimu katika shule.
“Tafiti zinaonesha kuwa bado kuna fikra zisizo sahihi kuhusu
masuala ya hedhi hususani miiko na unyanyapaa inayosababisha wasichana na
wanawake kushindwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kijamii
na wanafunzi wa kike kukosa baadhi ya siku za masomo na wengine kuacha shule
wanapokuwa kwenye hedhi. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
kulitambua hilo imeweka jitihada kuhakikisha kuwa fursa za elimu zinapatikana
kwa makundi yote,” Alieleza.
Halikadhalika mratibu wa mradi wa School Water Sanitation and
Hygiene (SWASH) Mwalimu Matinda Mwinuka aliwaasa waalimu kuhakikisha shule
zinakuwa na vyombo maalum kwaajili ya walemavu pamoja na vyumba kwaajili ya
wasichana kubadili pedi za hedhi pindi wanapokuwa katika hali hiyo nasio
kutumia vyoo vya kawaida ambavyo havina mazingira mazuri ya kubadilishia vifaa
vyao.
“Kuna shule moja fundi kaweka shule maalum, anasema kuwa kile
ndio chumba maalum, walemavu wataingia humo humo, hedhi salama wataingia humo
humo, ametoboa tundu na kuweka ‘pipe’ anasema Watoto wa kike wakishaingia humu
ndimo watatumbukiza vile vitu vyao yaani ni vitu vya ajabu kwakweli.”
Mradi huo unatekelezwa katika halmashauri tatu za Mkoa wa Rukwa
kwa muda wa miaka minne huku kwa mwaka wa fedha 2019/2020 Mkoa ulipewa kiasi
cha Shilingi 578,486,955.63/= kwaajili ya utekelezaji wa mradi huo
unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na kutekelezwa katika mikoa 17 na Halmashauri
86 za Tanzania Bara ukiwa na lengo la kuboresha mazingira ya kufundishia,
kujenga vyoo bora shuleni na kuweka miundombinu ya maji safi na salama.
Comments
Post a Comment