4/20/2021

WAZALISHAJI WA DAWA NCHINI WATAKIWA KUONGEZA KASI

Na WAMJW- Dar es Salaam.

Wazalishaji wa  dawa na vifaa tiba wote nchini wametakiwa kuongeza kasi ya uzalishaji dawa kwa kushirikian na Bohari ya Dawa(MSD) ili kuondokana na changamoto ya bidhaa hizo nchini.

Rai hiyo ilimetolewa Leo na  Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto- Afya Prof. Abel Makubi wakati alipotembelea Bohari ya Dawa na kuongea na wazalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini.

"Tunawashukuru kwa uzalendo wenu wa kuwekeza nchini, pokeeni  salamu kutoka kwa  Waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima na Manaibu Waziri".

Hata hivyo Prof. Makubi amewataka wazalishaji hao kushirikiana na MSD katika kuhakisha dawa zao zinawafikia wananchi wa vijijini ili kuweza kutatua changamoto ya Dawa Kwenye vituo vya kutolea Huduma za afya nchini.

Aidha, Katibu Mkuu huyo  amewahakikishia Wazalishaji hao kuwa Serikali ipo tayari kushirikiana nao na  kuhakikisha eneo la  uzalishaji dawa linakua ili kupunguza utegemezi wa dawa kutoka nje ya nchi.

"MSD ni chombo chetu Cha kuwatumikia wananchi hivyo ni vyema kukipa ushirikiano ili upatikanaji wa dawa,vifaa na vitendanishi ziwepo wakati wote".Alisisitiza Prof. Makubi.

Aliongeza kuwa ni wakati Sasa wa kuanza ukurusa Mpya kati ya Wazalishaji na MSD kwani utawala Bora  unajengwa kwa misingi ya Uzalendo, Uaminifu, na Kuaminiana .

Kwa upande wa Bei za bidhaa za Dawa, Katibu Mkuu huyo aliwataka Wazalishaji kukaa pamoja na MSD kupitia upya bei za bidhaa ili ziwe na uhalisia wa soko bila kuumiza Wananchi.

Licha ya hayo Prof. Makubi  amewaahidi kuwa  Serikali itawalipa kwa wakati Wazalishaji wote ambao watatoa ushirikiano wa kuleta dawa na vifaa kwa wakati na kwa ukamilifu. 

Nao Wazalishaji hao ambao ni wamiliki  wa viwanda vya dawa na bidhaa nyinginezo za afya nchini wameahidi kutoa ushirikiano kwa Serikali katika kuboresha upatikanaji wa dawa nchini na kuuunga mkono Serikali iliyoko madarakani inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.




 

    

0 comments:

Post a Comment