UZINDUZI WA MKUTANO WA WADAU WA AFUA ZA VVU NA UKIMWI DODOMA

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Protabas Katambi akikagua banda la Epidemic Control (EPIC) wakati wa Mkutano wa Mwaka wa wadau wanaotekeleza Afua za VVU na UKIMWI zinazowalenga wasichana Balehe na Wanawake Vijana unaofanyika leo April 29 jijini Dodoma.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Protabas Katambi akizungumza na Vijana wakati wa Mkutano wa Mwaka wa wadau wanaotekeleza Afua za VVU na UKIMWI zinazowalenga wasichana Balehe na Wanawake Vijana unaofanyika leo April 29  jijini Dodoma.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Protabas Katambi akikagua banda la Amref Tanzania wakati wa Mkutano wa Mwaka wa wadau wanaotekeleza Afua za VVU na UKIMWI zinazowalenga wasichana Balehe na Wanawake Vijana unaofanyika  April 29  jijini Dodoma. Picha na Raymond Mushumbusi WAMJW
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Protabas Katambi akikagua banda la Tanzania Youth Alliance (TAYOA) wakati wa Mkutano wa Mwaka wa wadau wanaotekeleza Afua za VVU na UKIMWI zinazowalenga wasichana Balehe na Wanawake Vijana unaofanyika  leo April 29  jijini Dodoma.
Baadhi ya Vijana waliohudhuria Mkutano wa Mwaka wa wadau wanaotekeleza Afua za VVU na UKIMWI zinazowalenga wasichana Balehe na Wanawake Vijana unaofanyika leo April 29  jijini Dodoma
.
 Na Raymond Mushumbusi WAMJW Dodoma
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Patrobas Katambi,amesema kuwa utafiti unaonesha  katika watu 72,000 wanaopata maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi  kwa mwaka asilimia 40 ni vijana na kati ya  hao asilimia 80 ni wasichana wenye umri kati ya  miaka 15-24.
Hayo ameyasema leo April 29,2021 akifungua mkutano wa mwaka wa wadau unaotekeleza afua za VVU na Ukimwi zinazowalenga wasichana balehe na wanawake vijana unaofanyika kwa siku mbili jijini Dodoma.

Mhe.Katambi amesema kuwa Katika utafiti huo watu 72,000  wanapata maambukizi mapya kwa mwaka na kati yao 40% ni vijana; kati ya hao vijana 80% ni wasichana wa umri wa miaka 15 – 24 ikimaanisha  kuwa kila kundi la vijana 10 wenye maambukizi 8 kati yao ni vijana wa kike na 2 ni vijana wa kiume.

 ''Ni  muhimu kuwahimiza vijana na watu wote kupima ili kujua hali zao, kutumia dawa kwa waliogundulika  na VVU na kuepuka maambukizi ikiwa bado hawajapata maambukizi''amesema Katambi

Aidha, Katambi amesema  kupitia matokeo ya utafiti wa 2016/17 Serikali iliona umuhimu wa kufanya jitahada za pamoja na wadau katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI, hususani katika kundi la vijana wa kike.

“ Nimeelezwa kuwa kuna juhudi zinazofanywa kupitia miradi ya DREAMS initiatives wenye lengo la kuwafikia mabinti balehe na wanawake vijana wenye umri wa miaka 15 - 24 wakiwemo waliozaa kwenye umri mdogo, wanaoishi na maambukizi ya VVU, wenye mahusiano na mpenzi zaidi ya mmoja, walioolewa katika umri mdogo, mabinti waliocha shule, na mabinti wanaoongoza kaya katika jamii na walio ndani ya shule”amesisitiza Katambi.

Hata hivyo Katambi amesema kiwango cha ushamili kimeendelea kupungua sambamba na kiwango cha maambukizi mapya na vifo vitokanavyo na ukimwi.

Amesema wastani wa kitaifa wa ushamili wa VVU ni asilimia 4.7 ambapo mkoa wa Njombe umekuwa kinara kwa kuwa na asilimia 11.4 ukifuatiwa na Mikoa ya Iringa asilimia 11.3,Mbeya asilimia 9.3 na Mkoa wa Dodoma maambukizi yameongezeka kutoka asilimia 2.9 hadi kufikia asilimia 5.

Pia Katambi ametaja miradi  inayolenga kutoa elimu ya kujikinga na VVU  kuwa ni pamoja na mradi wa  DREAMS unaotekelezwa katika Mikoa 4 Halmashauri (12), Mradi wa Ujana Salama unatekelezwa katika Mikoa 4 na Halmashauri (11) na mradi wa Timiza Malengo unatekelezwa Katika Mikoa 5 na Halmashuri (18).

 Katambi amesema kuwa '' Niwambie Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutekeleza miradi ya maendeleo inayolenga kuwalinda Wasichana Balehe na Wanawake Vijana na vijana kwa jumla kwa kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kijamii hususani kwenye kupunguza maambukizi ya VVU hasa kwa vijana ambao ndio nguvu kazi ya Taifa''amesema Katambi

Hata hivyo  Katambi amesema kuwa malengo ya nchi ni  kufikia sifuri ya maambukizi mapya ya VVU, sifuri ya ubaguzi na unyanyapaa utokaonao na UKIMWI na sifuri ya vifo vitokanavyo na UKIMWI ifikapo 2030. 

Kwa upande wake,Mkurugenzi Mkuu Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS),Dk.Leonard Maboko amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kuwaleta wadau na kuona wamefikia wapi na wamekutana na changamoto zipi pamoja na kuzitatua.

"Sisi TACAIDS kazi yetu ni kuratibu na ndio maana hapa kuna taasisi kazi yetu kubwa ya hili kundi ni kuratibu kila mwaka hivyo hichi kikao ni cha kuwaleta hawa wadau kuona wamefikia wapi na wamekutana na changamoto zipi pamoja na kuzitatua,ili kujadiliana tulipotoka tulipo na tunapoelekea,"amesema Maboko.

Dkt.Maboko amesema kuwa  Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa aliagiza Tacaids ifanye kazi na vijana ambapo alidai kwa sasa wanafanya kazi nao hususan wasanii.

Hata hivyo Dkt.Maboko amesema kuwa takwimu zinaonesha vijana ni kundi lenye Changamoto katika maambukizi ya Ukimwi.

"Tulianzisha Kijiji Maalum kwa vijana ambayo inalenga masuala ya vijana na haya yote yalikuwa ni maagizo ya Waziri Mkuu na yalitokana na

"Maambukizi mapya asilimia 40 yalikuwa yanatokea kwa vijana lakini asilimia 80 ya hao vijana ni wa kike,kwa umaalumu kabisa ndio maana hili kundi likapewa msisitizo huu.Takwimu zilituonesha hivyo tukaona kuna haja ya kuweka mkazo katika hili,"amesema

Awali ,Balozi Mwakilishi wa wasichana balehe na wanawake vijana Rosemari Shani akisoma risala amesema kuwa wanakabiliwa na changamoto za upungufu wa vituo vya kutolea huduma kwa vijana,ukosefu wa soko la uhakika wa bidhaa wanazozalisha,uelewa mdogo wa jamii kuhusu kinga za VVU.

"Elimu zaidi iendelee kutolewa tunaomba uziimize Halmashauri ziendelee kutoa mikopo kwa wanawake.Sisi Kama wasichana tunakuahidi kufanya juhudi kujiunga na Veta na Sido ili kukuza ujuzi.Tutaendelea kuwajibika katika familia zetu,"amesema 

Hata hivyo amesema kuwa  wanajivunia kumpata Rais mwanamke,Samia Suluhu Hassan kwani hiyo ni chachu kubwa kwao kuendelea kusoma na kufanya kazi kwa bidii.

"Tunajivunia kumpata Rais mwanamke jambo hili ni chachu kubwa kwetu.Tunaishukuru Serikali na wadau ambao wanatusaidia tunatarajia mambo mazuri,"amesema

Comments

Popular posts from this blog

CV YA KOCHA MPYA WA SIMBA PABLO FRANCO MARTIN "USIPIME"